WELCOME YOU ALL TO MY NEW BLOGS

Visiting this blog will help you to learn more about the laws of Tanzania and its related matters.

Sunday, April 22, 2012

HOTUBA YA MWALIMU JULIUS K. NYERERE MAY MOSI 1995. MBEYA




Nimeamua kuiweka hotuba hii kwenye Kona hii kwa kuwa ndani ya hotuba hii mwalimu ameongelea mambo mengi sana yanahusu sheria. Mfano Mwal ameongelea suala la siasa ya ujamaa na uhalali wake mpaka wakati huu, ameongelia sera ya ubinafshaji ambayo inagusa moja kwa moja mambo ya sheria ya uwekezaji na mwisho na kipengele ambacho ni muhimu kabisa kwa upande wa sheria ni pale anapozungumzia suala la Mgombea binafsi na kwa nini ni kinyume na haki za binadamu kupinga mgombea binafsi. Hivyo basi kama unataka kuyaelewa haya mambo vizuri likiwemo suala na ni kiongozi gani anayefaa kwa nchi hii nakualika usome hotuba hii maana baada ya kuisoma utabadirika sana kimtazamo na mawazo na utaungana na wengi wanaosema kuwa hotuba hii ni urithi wa taifa kutoka kwa hayati baba wa taifa kwa watanzania wa sasa na vizazi vijavyo.
John Mgayambasa.






TUMETOKA WAPI, TUKO WAPI,  TUNAKWENDA WAPI NA TUFANYE NINI ILI TUFIKE TUNAKOTAKA! 

HOTUBA YA MWALIMU JULIUS K. NYERERE ALIYITOA WAKATI WA KILELE CHA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI,
MBEYA MEI 1, 1995. 



Mwalimu Nyerere alialikwa kuwa Mgeni Rasmi kwenye kilele cha Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani iliyofanyika kitaifaUwanja wa Sokoine Mjini Mbeya Mei 1, 1995. Katika hotuba yake, Mwalimu alielezea historia ya Vyama vya Wafanyakazi duniani. Aidha alitumia fursa hiyo kutoa maoni yake kuhusu hali ya kisiasa na kiuchumi nchini pamoja na ushauri kuhusu mambo ambayo wananchi wanapaswa kuzingatia wakati wa Uchaguzi Mkuu mwezi wa Oktoba mwaka ule. Hasa sifa za wagombea nafasi za uongozi kuwa ni pamoja na kila mmoja kujiuliza ataifanyia nini nchi yake baada ya kuchaguliwa na anakwenda kufanya nini Ikulu? Ifuatayo ni hotuba ya Mwalimu.

Ni muhimu kukumbuka kuwa hotuba hii imefuata mlolongo wa mazungumzo ambayo Baba wa Taifa alikuwa nayo kwa wananchi katika maeneo mbalimbali ambapo alikuwa anajaribu kuamsha dhamira ya viongozi wetu wa wakati ule. Hotuba hii ni miongoni mwa hotuba ambazo ukweli wa hoja zake ni hazina kubwa kwa vizazi vijavyo vya Watanzania. 

Mwenyekiti wa OTTU, 
Viongozi wa OTTU, 
Viongozi wa Serikali, 
Viongozi wa Madhehebu ya Dini Mkoani na 
Wananchi wote wa Mkoa na Mji wa Mbeya. 

UTANGULIZI
Sababu za kukataa mwaliko wa mwaka uliopita na kuukubali mwaliko wa mwaka huu:

Kwanza kabisa, napenda kuwashukuru viongozi wa OTTU 
ambao walinijia na kuniomba nishiriki katika shughuli hii ya leo. Shukurani ya pili nataka kutoa kwa wananchi wa mjini Mbeya na mkoani Mbeya jinsi mlivyonipokea tangu jana mpaka leo. Ahsanteni sana. 
Ninyi siku zote, pamoja na mimi, tulikuwa tunazo tabia zetu za maadili ya kumwalika Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa ndiye awe Mgeni Rasmi katika shughuli hii. Kweli najua sasa taratibu zimebadilika, vyama vingi vya siasa, na kadhalika Lakini, hata hivyo, bado mnaweza Mgeni wenu Rasmi kuwa Rais. 
Mwaka huu hamkusudii mnakuja kunialika mimi? Sababu ya pili ya kukataa (mwaka jana) ni ile niliyowambia. Mwaka huu mmegomeana na Serikali. Sasa mwaka ambao mmefanya mgomo na Serikali kuja kuniomba niwe Mgeni Rasmi katika shughuli kama hiyo ndiyo tunatoa ujumbe gani? Ujumbe wa namna yo yote ile mimi siwezi kuutoa. Nilikataa.
 Nasema hizo ndizo sababu zangu za msingi za kuwakatalia mwaka jana na kuwakubalia mwaka huu. Vijana niliowakatalia ndio hawa. Sasa mwaka huu niwakatalie tena? Angalao hiyo ni sababu moja ya kuwakubalia mwaka huu. Huwezi kuwakatalia mwaka hata mwaka! 
Sababu yangu ya pili iliyonifanya nikakubali ni kwamba huu ni mwaka wa uchaguzi. Sasa, mwaka wa uchaguzi lazima wote tushirikiane kusema tunakwenda wapi? Nafasi kama hii ni nzuri kwa mtu ye yote mwenye mawazo kusema “jamani huu ni wakati wa uchaguzi tunakwenda wapi?”
Nikadhani ni nafasi nzuri mkinipa niitumie kutoa maoni yangu. Si yote. Ni baadhi, lakini ni sehemu ya maoni yangu katika jitihada za kusaidiana kuelewa tunatoka wapi, tuko wapi na tunakwenda wapi. Na kama tunataka kwenda huko, tufanyeje ili tufike huko. Tusije tukashtukia tunapelekwa mahala ambako siko tulikokuwa tunakusidia kwenda. 
Hizo ndizo sababu zangu kubwa za kuwa hapa. Hasa ya pili ndiyo iliyonifanya nikakubali kuja hapa. Kwa hiyo, kwanza ninawapongezeni ndugu wafanyakazi kwa siku ya leo, Siku ya Wafanyakazi Duniani. Tunaiadhimisha dunia nzima.

CHIMBUKO LA VYAMA VYA WAFANYAKAZI DUNIANI NA HAJA YA MSHIKAMANO 
Wazo la kuwa na vyama vya wafanyakazi duniani, kwamba wawe na mshikamano na umoja wa kutetea maslahi yao sio wazo la Tanzania wala la nchi zilizoendelea. Kusema kweli, kwa historia, lilianza huko Marekani na lilikubalika. 
Wafanyakazi wa wakati huo, katika nchi ambazo maendeleo yake yalikuwa mazuri, waliamua wafanye mshikamano wa kuleta maendeleo yao na hasa ya kupambana na waajiri wao.
Mwajiri anaanzisha shughuli yake na anafanya kwa nguvu zake mwenyewe. Anataka kulima na analima kwa nguvu zake mwenyewe. Kama anataka kufungua kiwanda chake cha mbao, maana ninyi ni wafanyakazi inapasa nizungumzie habari ya viwanda badala ya kilimo, anafungua kiwanda chake cha kutengeneza samani. Anaweza kutumia vitu vyake mwenyewe na akawa anafanya kazi na seremala mmoja. Atakuwa amepata randa, meza, patasi na kila kitu chake. 
Anafanya kazi yake mwenyewe, anatengeneza vitu vyake, anauza na anapata hicho anachokipata. Hicho anachokipata kinatokana na nguvu yake mwenyewe. Anataka mbao na anatengeneza. Mtu anamwendea na kumwambia, “mimi nataka meza bwana”, anamtengenezea. 

Inabidi mwenyewe ashughulike na meza hii mpaka inakuwa nzuri. Anapata kile anachopata. Nyingine anafidia zile gharama zake za meza, randa na za vyombo vingine vyote hivyo. Halafu, kinachobaki cho chote, ndiyo maslahi yake. Lakini, kile anachopata kinatokana na jasho lake mwenyewe. Akitoka hapo, anaweza kuwa mshiriki na mwenzake, washirikiane wote wawili na sio kwamba mmoja atamwajiri mwingine. Hapana! Wote wawili watafanya kazi kwa pamoja. Watasaidiana vizuri zaidi wakifanya pamoja. Wao, vile vile, wanaweza wakapata maslahi kutokana na nguvu zao wenyewe. 
Mwanzo wa dhuluma ya unyonyaji 
Wakitoka hapo nao wakajifanya ni waajiri wanaotaka kuwaajiri wengine, shughuli ile si ya hawa walioajiriwa tena. Ni ya hawa wawili tu. Wakisha kuwaingiza wengine, hao si yao. Wanasema. Sasa njoo hapa tusaidie kutengeneza meza, vitanda, madirisha na milango. Lakini, meza inapokuwa imekwisha, tunaiuza. Si mali yenu ninyi wafanyakazi. Ni mali yetu. Ninyi chenu humu ni ule mshahara na wala sio faida itakayopatikana humu. Faida, [baada ya kutoa gharama zote za ununuzi wa mbao, usafirishaji wa mbao zote zile pamoja na gharama za kuwaajiri ninyi mwitoe meza hii - kwa kuwa mishahara yenu ni sehemu ya gharama] nikitoa gharama zote hizi, kinachobakia ni changu. 

Sasa ile inayobaki, baada ya kutoa gharama hizo, inaweza kuwa kubwa na inaweza kuwa ndogo. Inategemea sana gharama zilikuwaje. Kama gharama za kununulia mbao zilikuwa kubwa, zinanipunguzia faida yangu. Kama gharama za wafanyakazi ni kubwa mishahara ya wafanyakazi kama ilikuwa mikubwa, inanipunguzia faida yangu. Kwa hiyo, sipendi vyote viwili. Sipendi muuza mbao aniuzie aghali na sipendi mfanyakazi adai mshahara mkubwa. Napenda wote waniuzie rahisi. Nataka mbao kiurahisi, nataka mishahara iwe chini. Hapo ndipo ninapopata faida kiuchumi. 
Hili sijambo la ajabu la wazungu wenzetu wanaojua bali ni la kila mtu mwenye akili kama zenu kutokana na mtiririko wa mantiki wa hoja yenyewe. Kwamba, mimi nataka mshahara wenu uwe mdogo kwa kuwa faida yangu inatokana na mshahara wenu kuwa mdogo. Sasa ninyi mtasema: ALAA Bwana Mkubwa, kazi tufanye sisi halafu wewe utupe mshahara mdogo. Tukufanyie kazi wewe? Basi uone iwapo tutakufanyia. 

Umoja na mshikamano ndio silaha va kupambana na dhuluma ya unyonyaji
Kama watakuwa wananiambia mmoja mmoja, nitawafukuza. Unakuja peke yako na unaniambia Lakini Mzee sasa mimi nataka uniongeze mshahara. Nitakuambia. Unaniambia nini wewe? Unasema nikupe mshahara wa shilingi ngapi? Utajibu. Ah, kama utakavyoona, lakini uniongeze. Mungu anaona na Mtume. Nikaona kidomodomo chake huyu Nikamuambia: Unataka mshahara huo ninaokupa sasa hivi? Nyamaza na nenda kafanye kazi huku utachagua. Kama hutaki, toka. Kazi sikukuomba. Ulikuja mwenyewe. 
Nitakutisha hivyo. Ukifikiri mchezo, nitakufukuza. Na wenzako watajua kafukuzwa kwa nini yule. Amedai mshahara mwingi. Mimi kimya! Wengine hawatathubutu tena maana watafikiri. Nikisemasema hapa na mimi nitatimuliwa na watoto wana njaa. Nikitimuliwa nitapata taabu. Wewe unaonaje? Anaendelea huyu kukunyanyasa. Kama anaweza kuwanyonya wauza mbao na kukunyonya wewe mfanyakazi, atawanyonyeni wote mpaka wauza mbao washirikiane kwa pamoja wapate bei nzuri. Mpaka wafanyakazi washirikiane kwa pamoja wapate mishahara mizuri. Bila kushirikiana, hawapati mishahara mizuri. 
Hii ndiyo asili ya kuanzisha Vyama vya Wafanyakazi. Nasema hamkuvianzisha ninyi vilianzishwa zamani, tena Marekani. Lakini, Marekani havikuwa na nguvu sana. Vilikuwa na nguvu zaidi Ulaya. Hata hivyo, havina nguvu sana tena Ulaya. Sitaki kuingilia na kuliendeleza hili kwa kuwa viongozi wenu kama wanaelewa, watawaelezeni.
 Zamani, Vyama vya Wafanyakazi vilianzisha mshikamano wa Wafanyakazi Duniani. Kauli mbiu yake ilikuwa Wafanyakazi Duniani Unganeni. Hamna cha Kupoteza isipokuwa minyororo yenu. Mantiki ya kauli mbiu hiyo i1ikuwa kwamba, kwa kuwa mmefungwa minyororo na mmenyonywa unganeni. Huo ulikuwa ndio ujumbe wa kauli mbiu hiyo kwa Wafanyakazi Dunia nzima. Hata hivyo, sisi hatukuwapo. 

TUMETOKA WAPI?
Hatukuwa wamoja
Hii ni nchi mpya na ndiyo ambayo tumekuwa tunajaribu kuijenga. Kwanza Tanganyika, kwa muda mfupi na, halafu, Tanzania. Kusema kweli, sisi wengine maisha yetu ya urais wetu ni wa nchi inayoitwa Tanzania. 
Nilipokuwa rais wenu, ni1ifanya juhudi za kukomboa eneo hili linaloitwa Tanganyika. Lakini, uongozi wangu niliowaongoza ninyi katika nchi huru inayojitawala na raia duniani wa nchi huru inayojitawala. Niliwaongozeni katika nchi inayoitwa Tanzania. Tanganyika niliwaongozeni kwa muda mfupi tu; tangu Disemba 1962 mpaka Aprili 1964 basi. Kipindi changu kingine chote, niliongoza nchi inayoitwa Tanzania siyo Tanganyika. Kwa kweli, siijui Tanganyika ya watu huru. Ni muda mfupi mno. 
Nchi hii Tanganyika, ni nchi changa. Watu wake waliwekwa katika sehemu inayoitwa moja na Wajerumani. Wamakonde na Wazanaki hawakuwa wamoja. Waliwekwa pamoja na Wajerumani ili watawaliwe. Jitihada ya kuwafanya wawe pamoja na kuanza kusema “Ninyi ni Wamoja” haikufanywa na Wajerumani. Hakuna Wajerumani ambao wangeweza kusema “Ninyi ni Wamoja” kwa kuwa lengo lao halikuwa kujenga umoja. Wajuremani walichoweza kusema ni kwamba “Ninyi ni Tofauti, Ninyi ni Tofauti!” ili waendelee kututawala. 
Jitihada ya kwanza ya dhati ya kusema “Ninyi ni Wamoja” ilikuwa ni yetu sisi tulipoanzisha chama cha TANU. Shabaha yake kubwa ilikuwa ni kujaribu kujenga umoja ili tuwatimue Waingereza. Lakini mbinu yake ya kwanza kabisa iliyotajwa ilikuwa ni kufuta ukabila. “Sahau Ukabila!” tulitamka kwa ukali. Wale ambao, labda mpaka leo, wanako kakitabu ka milango ya historia ka Katiba ya TANU wataona tumeshambulia kitu ukabila. Tukaanza hatua ya kwanza kabisa, kusema “Sisi ni Taifa”. Lakini halikuwa likiitwa taifa la Tanganyika. 
Tujenge misingi va umoja ili tuelewane na tujuane kuwa ni wamoja na ni ndugu
Nataka kusisitiza nini: Kwamba sisi ni taifa changa miongoni mwa mataifa machanga. Taifa hili halijajenga mizizi mirefu ya kuwa taifa huru kuwakaribia Waingereza. Waingereza wana miaka mingapi? Sijui, labda elfu na zaidi. 
Katika mataifa machanga duniani, moja ni Marekani. Lakini, Marekani wana miaka mia mbili na zaidi ya kuwa taifa. Vitaifa vingi vya Ulaya vina miaka mingi tu! Mataifa machanga haya lazima yajenge misingi inayowafanya raia wake wajiite sisi. 

Tumejitahidi na ndivyo jitihada zetu zilivyokuwa. Lakini ukijenga nchi moja, unajenga misingi ya umoja ili tuelewane na tujuane kwamba sisi ni wamoja, ni ndugu. Kama tunahangaika kufanya kazi hapa, tunahangaika kwa pamoja. Kama tunahangaikia ulinzi, tunalinda nchi yetu kwa maslahi yetu pamoja.
Tunaulizana “nini mahitaji yenu?” Tunajitahidi wote, tunayapata. Kama tunataka elimu, tunasaidiana wote tupate elimu. Siyo tuseme kwamba wengine wapate elimu wengine wasipate. Kama tunataka afya, tunataka kujitahidi wote tuweze kutafuta njia kusudi wote wote tupate afya, wote tuwe na afya. Siyo wengine wapate afya wengine wasipate. Kama tunataka nyumba nzuri, wote tujitahidi kwa pamoja tuone kwamba tunajenga mazingira wezesha yatakayohakikisha kuwa kila Mtanzania atakuwa na nyumba nzuri kwa pamoja. Hapo ndipo tunaweza kushirikiana tujenge nchi pamoja.

Azimio la Arusha na Siasa ya TANU ya Ujamaa na Kujitegemea
Tukaweka kitu kimoja hapa kinaitwa Azimio la Arusha. Leo narudia kusoma Azimio la Arusha hata kama hamlitaki. Kama kuna watu Tanzania hawajali, wachukue waanze kulisoma ili waone na waniambie wanachokiona mle kibaya ni nini hasa. Asome tu kwa dhati tu na kisha aseme hiki ni kibaya.
Siasa va Ujamaa
Linasema Azimio la Arusha, kwa msingi kabisa, kwamba “Nchi.yetu ni ya Wakulima na Wafañyakazi”. Sasa mnasemaje? Imeacha kuwa ni nchi ya Wakulima na Wafanyakazi? Kwa hiyo, kama tunaijenga nchi hii, tunaijenga kwa faida ya Wakulima na Wafanyakazi. Ndivyo Azimio Ia Arusha linavyosema. Ukweli huo umekwisha? Umefutika? Umefutwa na nani? Nini kimefuta ukweli huo kwamba nchi hii ni ya Wakulima na Wafanyakazi? Ninyi hapa ni Wakulima na Wafanyakazi. Mtaona wafanyabiashara wadogo wadogo, siku hizi wengine wanaitwa Wamachinga. Lakini, hasa hasa, nchi hii bado ni nchi ya Wakulima na Wafanyakazi. Kama tutafanya jitihada za kuijenga nchi hii, tutajenga uchumi wake na huduma zake za umma ambazo lazima ziwafae Wakulima na Wafanyakazi. Hali hiyo imebadilika lini? 
Siasa va Kujitegemea
Tukasema kwamba “Hatuna budi kujenga nchi hii kwa kujitegemea”. Hatuwezi kuwa tunataka maslahi yetu ya Watanzania ya afya bora, maisha bora na elimu nzuri lakini eti tudhani tunaye mjomba huko nje atakuja kutuletea maslahi hayo. HATUNA! Tutajenga nchi hii kwa faida yetu wenyewe sisi wenyewe. Akipatikana mtu kutusaidia, tutamshukuru. Lakini kazi ya kujenga nchi hii kwa manufaa ya Watanzania wote ni kazi ya Watanzania, si kazi ya mtu mwingine. Msimamo huo tukauita Siasa ya Kujitegemea. 
Msingi huo umekufa. Hivi mmeshapata mjomba? Hivi kweli mtawadanganya Wafanyakazi hawa msiwambie “chapeni kazi kama mnataka maslahi yenu yaboreshwe, tuchape kazi kwa faida yetu!” Tuache kuwambia wakulima kwamba “kama tunataka maendeleo, tuchape kazi hivyo hivyo”. Hivi mtawambia hawa kwamba “tumeshapata mjomba msiwe na wasiwasi!” Mjomba huyo ni nani? Mimi nitafurahi kumwona. Nitakwenda kumwona, lakini sitamwuliza lo lote. Nitafurahi kumwona. Halafu mkinionyesha, “ndiye huyu mjomba”, nitacheeka!! Hali ya nchi hii haijabadilika hata kidogo. Tanaweza kujenga nchi kwa maslahi ya Watanzania kwa siasa ya kujitegemea tu, lakini kwa manufaa ya wote. Manufaa ya wote ndicho tulichokiita ujamaa. 
Nchi ya Kijamaa
“Nchi ya Ujamaa”, tukasema, “ni nchi ambako kila mtu anafanya kazi. Kama ni mkulima, anafanya kazi; kama ni mfanyakazi, anafanya kazi”. Lililokuwa la msingi na linalotawala ni mfanyakazi: maslahi yanatokana na kazi yake na jasho lake. Watu ambao hawana ulazima, kimsingi ya kupata maslahi yao kutokana na jasho lao wenyewe wapo. Watoto wadogo hawana jukumu hilo. Eti chakula chao kitokane na nguvu zao wenyewe? Hao ni wanyonyaji wa haki sawa kwani wanawanyonya mama zao. Ni haki yao. Lakini zee na madevu yake hatulitazamii limnyonye mama yake. Watoto wadogo tu wanayo haki hiyo. Vile vile, kuna watu ambao hawana uwezo wowote ule wa kujifanyia kazi- sio uwezo wa kutokuwa na kazi! Wako watu hawawezi. Wana vilema fulani ambao hawawezi kufanya kazi wajipatie riziki kwa kazi na kwa nguvu zao wenyewe. Hawa wana haki ya kulishwa na kutunzwa na umma pamoja na jumuiya zote. Hali kadhalika, wako watu wazima ambao wamefanya kazi zao. Walipofika umri wao wa kushindwa, hawawezi kufanya kazi tena. Ah, basi tena. Hawajiwezi hawa, tuwatunze. Hawa ni haki kuwatunza. Wamo watu wa aina hiyo wanajulikana kila mahala. 

Nchi ya Kibepari
Hata hivyo, mbali ya makundi hayo, wapo watu wengine ambao wanapata riziki yao kwa kufanya kazi na wengine wanapata riziki yao kwa kafanyiwa kazi. Nasema nchi ya namna hiyo inaitwa ya kibepari. Nchi inakubali wengine wafanye kazi na kupata riziki yao kwa jasho kama inavyosema misahafu, wengine wanafanyakazi kwa kunyonya kama watoto wadogo kama vile vilema na vizee. Ni majitu yanakaa na uwezo wao yanatumia wengine kama vyombo. Kwa hiyo, mfanyakazi na randa ni sawa sawa. Nasema nchi ya namna hiyo inaitwa ni nchi ya kibepari. Sasa katika dunia ya siku hizi maneno hayo si mazuri sana kuyasema. Na mimi nawakumbusheni tu na wala sijayasema! Mimi sina taabu, nawakumbusheni tu. Hill Azimio la Arusha, ambalo sasa mnalitemea mate, lilikuwa linasema hivyo na, kutokana nalo, kuna mambo fulani tukaanza kuyapata.

BAADHI YA MATUNDA YA AZIMIO LA ARUSHA
Moja ya mambo yanayopaswa kuzingatiwa ni la hali yetu mbovu ilivyokuwa kwanza wakati tunajitawala. Nchi tuliyoipokea kutoka kwa wakoloni ilikuwa ni masikini sana. Ilikuwa nyuma kabisa kwa upande wa elimu. Tulipojitawala, tulikuwa na wahandisi wawili. Kijana mmoja aliitwa Mbuya na alifariki katika miaka miwili hivi baada ya kujitawala. Tulikuwa na madaktari kumi na wawili wakati tunajitawala mwaka wa sitini na moja. 

Kujenga uçhumi wa viwanda
Tukaanza shughuli ya kujenga uchumi wetu. Natumaini nitazungumzia hili la viwanda. Nchi zinazoendelea duniani [kama Marekani ya Kaskazini, Marekani yenyewe na Kanada, Ulaya, hasa Ulaya Magharibi na Japani] na maana moja ya kuendelea ni kwamba uchumi wake unategemea viwanda. Viwanda ndivyo vinatengeneza vipaza sauti, kamera zetu tunazotumia sasa nakadhalika. 
Maana ya maendeleo ya leo ya uchumi wenye nguvu ni maendeleo ya viwanda. Nchi yenye viwanda tunasema ni nchi iliyoendelea. Hata hivyo, tuna maana nyingine ya nchi zilizoendelea ya kuziita ni nchi zenye viwanda. Nchi haiwezi kuendelea bila kuwa na viwanda vya kisasa. 
Viwanda vya nguo ndio rahisi kuanza navyo:  historia ya utawala wa Waingereza India 
Wakati tunajitawala, hatukuwa na viwanda. Tulikuwa tunalima kahawa, mkonge na pamba, lakini tunanuza vyote nje. Mimi najua kidogo historia ya Uingereza, ilikuwa ndiyo nchi ya kwanza duniani kuanza maendeleo ya kisasa ya viwanda. Sekta moja ya viwanda walioanza nayo, ambayo ilikuwa rahisi wakati huo na leo ni rahisi zaidi, ilikuwa ya kutengeneza nguo. Waingereza wakaitumia na wakajenga viwanda. Nguo zao zikawa zinatokana na viwanda vyao. 
Vile vile, walikuwa wana dola kubwa. Walikuwa wanatutawala sisi Afrika, wanawatawala Asia na wanatawala sehemu nyingine za Amerika, lakini hasa Afrika na Asia. Walipoingia India, walikuta Wahindi tayari wanatengeneza nguo zao kwa mashini. Wakawaza “hata Wahindi nao wanatengeneza nguo! Haina maana”. Wakawazuia Wahindi kutengeneza nguo kusudi soko duniani liwe la Waingereza: liwe huru lisizuiwe zuiwe. Namna moja kulifanya soko hilo kuwa huru ilikuwa ni kwa kuvitawala vijitu hivi, halafu unauza vitu vyako. Wenyewe ndivyo walivyoanza na viwanda vya nguo na, baadaye, wakaongeza vingine na hatima yake, Waingereza wakawa wakubwa. Wenzao duniani wakaona  “Alaa hivi Vingereza tunaviachia vinaendelea namna hii kwa nini?”. Wakaanza mambo, wakagombana gombana, wakapigana pigana na wakanyang’ anyana. 
Tulipojitawala mwaka sitini na moja tulikuwa tunajua mambo haya, ijapokuwa tulikuwa wachache, kwamba nchi haiwezi kuendelea na kuwa ya kisasa bila viwanda. Mtawachumia pamba wakubwa hawa na kukata miwa. Hiyo ilikuwa sababu moja ya kuleta utumwa ili kuwachukua Waafrika waende Marekani wakachume pamba na wakakate miwa.
 Baada ya kupata uhuru tukajiuliza. Leo tunajitawala, tuendelee kuchuma pamba na kukata miwa? Tukaamua: Tuanze kujenga viwanda kwa kuwa sisi tunalima pamba. Kwa hiyo, shughuli ya kwanza kabisa tutakayoanza nayo ni ya kujenga viwanda vya nguo. 
Nikawaomba wanaojua mambo haya ya viwanda duniani. Wakati huo sisi wenyewe hatukuwa na watalaam. Nikawaeleza watu hawa maneno haya: Hivi tunajitawala, tuendelee kuuza pamba ghafi nje? Nataka nianze kutengeneza nguo hapa Tanzania.
 Wakanishauri na wakaniambia Mwalimu, mnaweza kuanza kutengeneza nguo kutoka pamba yenu hapa. Jenga uwezo ili Tanzania iweze kutumia asilimia themanini na tano (85%) ya pamba inayolimwa Tanzania kutengeneza nguo hapa hapa. 

Walinishauri nijenge uwezo ndani ya Tanzania wa kutumia asilimia themanini na tano (85%) ya pamba yetu hapa hapa. Asilimia kumi na tano (15%) ya pamba iliyobaki, ama tunaweza tuitumie wenyewe hapa hapa au tunaweza kuiuza nje. Hiyo ilikuwa safi sana, kwamba tujenge viwanda kwa makusudi kabisa.
 Wakati ule, hata mimi ningekuwa na sera za kibepari, ningejenga viwanda. Mabepari ndio walioanza viwanda na viwanda vyenyewe hivyo havikuwa na sera ya ubepari au ujamaa. Vilikuwa ni viwanda tu! Sasa tukaanza kujenga viwanda vya nguo na sasa sitaki kusema sana juu ya jambo hili.

TUKO WAPI – MAKOSA YA UBINAFSISHAJI WA MASHIRIKA YA UMMA
Juzi juzi, wakati nipo pale Dodoma, vijana walinikumbusha. Mwalimu, ulipotoka, uliacha viwanda vya nguo vya umma kumi na viwili. Kati ya viwanda hivyo kumi na viwili, kumi vimefungwa na viwili vilivyobaki kimoja hatujui hata kama kitapata pamba. Tusipoangalia, vyote viwili vilivyobaki vitafungwa. 
Juu ya Mashirika ya Umma
Nataka kusema kidogo juu ya hiki kitu kinachoitwa mashirika ya umma. Sijui yananuka? Hata hivyo, hata kama yananuka, nataka kujua kwa nini yananuka. Lazima tujiulize kwa nini yananuka. Sababu ya kusema hivi ni kwamba mimi nilikuwa sijui, lakini vijana walinikumbusha wakaniambia “Mwalimu, ulipondoka, uliacha kumi na mbili”, Mimi kitu kimoja nilichokuwa nakifikiria ni kwamba sasa viwanda vyetu vya nguo vilikuwa vinafikia shabaha ile tuliyokuwa tunataka ya kuweza kutumia asilimia themanini na tano (85%) ya pamba hapa nyumbani. 
Nilipowauliza vijana kwa nini viwanda kumi vimefungwa na viwili vilivyobaki vipo katika hatari ya kufungwa, nilielezwa kwamba kuna sera inayoitwa sera ya ubinafsishaji. CCM wasiogope sana, na ninyi mniwie radhi kwa kusema CCM, maana ndiyo yenye serikali inayotawala. 
Sasa mimi nifanyeje? Wala CCM wasije wakaninung’ukia, maana ndicho chama kinachotawala, na wale wa vyama vingine wasije wakasema “Mbona Mwalimu umesema kama unaipendelea CCM? Aka! Kama wanataka niwabomoe, naweza kuwabomoä, lakini sitaki. 
Mimi nataka kueleza hali yetu ilivyo hivi sasa na nataka kusema, mosi, tunatoka wapi, tuko wapi na tunataka kwenda wapi, Pili, kama tunataka kwenda huko, tufanye nini tusije tukashtukia tunapelekwa mahala ambako siko tunakokusudia kwenda. Na hiyo ndiyo shabaha yangu. 
CCM imebadili sera ya Azimio la Arusha
CCM imebadili sera ya Azimio  la Arusha. Mimi sina ugomvi hata kidogo. Naweza kusema nina ugomvi wa kiitikadi, ingawa sijasema “mbona mnaacha sera yetu ina ubaya gani?”. Aidha sina ugomvi wa msingi wa kitaifa kwa sababu mnaweza mkaacha Azimio la Arusha na baadae mkajenga uchumi imara tu kwa manufaa ya wananchi. Ziko namna nyingi za kufanya hivyo na si lazima kufuata Azimio la Arusha. 
Sera za CCM
Sasa CCM wanazo sera ambazo zimefafanuliwa katika kakitabu haka kanakoitwa Mwelekeo wa Sera za CCM katika Miaka ya Tisini. Hii imetengenezwa na ndio marekebisho ya Azimio la Arusha. Ndiyo sera yao mpya baada ya kusahihisha Azimio la Arusha. Kuna sehemu ninayotaka kuitumia kueleza hayo ninayotaka kuyaeleza ambayo inahusu mashirika ya umma.
Sera ya ubinafsishaji wa mashirika ya Umma
Kuhusu mashirika ya umma, sera yake inasema. “Mashirika ambayo ni ya msingi na nyeti kwa maendeleo ya taifa kama bandari, reli, posta ma simu, nishati na mabenki ya umma yaliyopo, yaendelee kumilikiwa na dola. Hata hivyo, wananchi wataweza kuuziwa sehemu ya hisa katika mashirika hayo yote na mashirika haya yanaweza kuingia ubia na makampuni binafsi, mradi tu kwa uwiano unaolifanya shirika kuendelea kuwa la dola”. Mimi nilipokuwa nasoma jana nikaafiki na kukubali. Sina ugomvi na hilo na sina ugomvi kabisa kwani ndivyo tulivyosema katika Azimio la Arusha. Lakini mambo haya lazima yabadilike. Sasa sina ugomvi na hili.

Pili: “Mashirika ya umma ambayo yanaendelea kwa ufanisi lazima yaendelee kuwa ya dola kwa lengo la kuendelea kuwashirikisha wananchi katika umilikaji. Mipango itaandaliwa ya kuwawezesha wananchi kununua hisa katika mashirika hayo. Pia mashirika ambayo yanahitaji mtaji au kupenyeza sayansi na teknolojia ya kisasa yataweza kuingia katika ubia iili kutimiza azma hiyo. Aidha kwa mashirika ambayo serikali italazimika kumiliki, mashirika haya itabidi yaendeshwe kibiashara”. Mimi nakubali mia kwa mia, sina maneno na wala sioni tatizo na hilo.

Tatu: “Kwa upande wa mashirika ambayo yanaweza kufanya shughuli zake kwa faida lakini yana matatizo mbali mbali kama ya ukosefu wa mtaji, madeni makubwa katika mabenki, menejimenti mbovu na kadhatika, dola itachukua hatua ya kulazimika kuondoa menejimenti mbovu, kuimarisha mtaji kwa kuwauzia wananchi hisa na kuingia ubia na vyombo vingine vya kiuchumi au kuyakodisha kwa mteja mwenye uwezo wa kuyaendesha kwa faida”. Mimi hiyo bado naikubali na sina matatizo.

Nne: “Mashirika yaliyo sugu [“mashirika yaliyo sugu” tena Kiswahili kizuri sana] kwa kufanya shughuli kwa hasara yatakodishwa, ama kuuzwa au kufungwa kwa kutilia maanani  zaidi jawabu ambalo ni la maslahi zaidi kwa taifa”. Sasa mimi nasema hilo bado nalikubali kwani shughuli hii imekuwa inaendelea. Nimesikia kwamba shirika, halikuwa ni shirika la umma, lilikuwa ni Benki ya Ushirika na Maendeleo Vijijini (CRDB), peke yake ndicho chombo cha namna hiyo ambacho kimepitapita kuuza hisa. Mengine sijayasikia, yanaweza kuwa yapo.

Uuzaji wa mashirika ya umma
Uuzaji wa mengine, ambayo sivyo sera inavyosema [sera haisemi mashirika yanayoendeshwa kwa faida yauzwe hata kidogo], sijui yanavyouzwa. CRDB wamepita kwangu pale wameniomba ninunue hisa. Nitapata wapi mimi? Hata hivyo, wamepitapita wanaomba watu wanunue hisa; wanakwenda kwenye vyama vya ushirika na wanawaomba watu binafsi. Angalau, hicho ni kitendo cha kushirikisha watu ambacho wamekifanya na watu wametumia fursa hiyo kama sera inavyosema. 

Mengine tunasikia yanakwenda tu. Eti sasa ni kwamba, kwa mfano, kile kiwanda cha sigara, ni cha umma ni chetu wote pamoja. Najua wewe huna hisa, mimi sina hisa na wala hakuna mtu mwenye hisa. Lakini ni cha umma na kinafanya shughuli zake kwa faida. 

Tofauti kati va shirika ya umma na shirika/kampuni binafsi

Nimechukua mfano wa kiwanda ambacho kinafanya shughuli zake kwa faida. Kama kinafanya shughuli zake kwa faida, wote tunapata faida. Chukua mfano wa viwanda viwili vinavyoendeshwa vizuri na vinapata faida. Kimoja kama kile cha sigara na cha pili ni cha watu binafsi. Sasa tofauti yake ni nini? Hiki cha watu binafsi kinalipa kodi ya serikali na hiki cha umma kinalipa kodi ile ile na kwa mujibu wa sheria ile ilee. Kwa hiyo, hivyo vyote vinalipa kodi ile ile juu ya faida kwa asilimia ya faida zao kwa mujibu wa sheria. Baada ya kodi, pato lililobaki linagawanywa kwenye hisa. Kile cha umma pato lake linakwenda kwa serikali: kwa umma. Hiki kingine, faida yake inakwenda kwa watu binafsi wachache. 

Ndiyo maana, mpaka leo, mimi napendelea hiki cha umma zaidi kuliko kile cha watu binafsi. Vyote vinafanya biashara nzuri tu na vinalipa kodi ya serikali kama kawaida na vinawapa faida iliyobaki wenye kiwanda. Hata hivyo, hicho cha kwanza, cha umma kinawapa faida iliyobaki wenye kiwanda hicho ambao ni umma, na msimamizi wake ni serikali. Kwa hiyo, serikali ndiyo inayochukua mapato yake kwa niaba ya wananchi wake. Mimi mpaka leo, hata ninyi mngesemaje, bado nakipenda hiki cha umma. 

Tukitaka kuongeza viwanda vya watu binafsi, tuongeza tu!
Kama tunasema sasa hivi tunataka kuongeza vile viwanda vya watu binafsi, tuongeze tu! Nani atatuzuia? Ongezeni vile vya watu binafsi. Viongezwe kwa wingi kabisa! Hata hivyo, mnapochukua hiki cha umma, kwa maana niliyoieleza, mkasema eti mnataka sasa kiwe cha wananchi moja kwa moja ili na mimi Nyerere niseme “sasa nina hisa pale”, mimi siafiki. Watu wangapi mtakuwa na hisa? Hebu niambieni, wangapi? 

Mnachukua mali yetu wote kabisa, kiwanda cha sigara kile kina mali, kinapata faida na serikali inaitumia kuongezea fedha za kodi na tunaifanyia kazi ya umma. Mnavyosema leo ni kwamba mmegundua njia moja nzuri zaidi ya kushirikisha wananchi katika uchumi. Mimi nawambineni: ongezeni viwanda.

Muwashawishi wananchi wa Tanzania waongeze viwanda. Wasaidieni kuongeza viwanda. Lakini, hiki cha wote, mnataka kuwapa watu wachache, halafu mnasema ndio ushirikishaji? Mimi sielewi maana yake. Hii ni mali yetu wote pamoja: ni mfuko wa pamoja tunachota inatusaidia katika elimu, afya na mahitaji mengine. 

Sasa hivi tunayo matatizo ya ukusanyaji kodi. Kiwanda hiki hakina matatizo hata kidogo. Kinaendeshwa vizuri kwa faida. Kwa hiyo, tunacho chombo ambacho kinatoa faida. Kinatusaidia. Leo shule na hospitali zina matatizo kwa sababu kodi mbali mbali hazikusanywi. Lakini kiwanda hiki kinalipa kodi yake kama kawaida. Miongoni mwa wale wanaokwepa kulipa kodi, si mmoja wao. Viwanda vya umma si mmoja wapo hata kidogo. Vinalipa kodi zake kama kawaida, havikwepi kulipa hata senti moja. Halafu, kinapopata faida, tunabaki nayo na tunafanya shughuli za wananchi. Hiki mnasema leo tukigawanye tuwashirikishe wananchi kwa kukimiliki moja kwa moja. Wangapi mtamiliki: ninyi wangapi? Itakuwa ni kuchukua fulani na fulani tu! Kiwanda ambacho ni chetu wote kabisa na faida itakapobaki, badala ya kwenda Hazina, iende kwa wewe na mimi! 

Ndiyo tumekibinafsisha na hii ndiyo sera mpya ya kuleta manufaa Tanzania! Hii ndiyo mbinu mpya imegunduliwa? Ujamaa mpya huo! Huo ni unyang’anyi tu wa mali yetu wote. 

Kutegemea mtu mwingine kwa mawazo ni kubaya kupita yote kabisa
Hili ni jambo la upumbavu. Katika masuala ya uchumi wa nchi, lazima tufanye tofauti baina ya kujitajirisha wachache na kuleta manufaa ya watu wengi. Sasa, sera hii itazaa mamilionea sasa hivi na sio baadaye, lakini watakuwa mamilionea watano. Hata hivyo, wakati huo huo, pia itazaa masikini na Tanzania itakuwa na masikini wengi sana.

Sasa nataka niseme kuwa nimetumia kiwanda cha sigara kama mfano tu kuonyesha kwamba nchi haiwezi kuendelea hata kidogo kwa kupuuza viwanda. Sasa tunafunga viwanda. Sijui hiyo inaitwa sera ya kuondoa ama kuzuia viwanda, lakini haya ni matatizo ambayo tunayo na usifikiri ni Tanzania peke yake. Nilikuwa Mwenyekiti wa Tume ya Kusini nimepita pita Afrika, Asia na Amerika ya Kusini. Nimeshuhudia mawazo na mipango ya aina hiyo kuwa ndiyo inayoongoza na kutawala. Hilo ndilo nililowambia hivi punde kwamba, wakati Waingereza wanatawala India, waliwaambia Wahindi. “Hapana kutengeneza nguo.”
Hali hiyo inaendelea na wala haijabadilika mpaka leo kwani bado duniani tunaona nchi zenye viwanda huvibana viinchi vidogo viache mambo ya viwanda. Sasa taabu yetu, wala si Tanzania peke yake kuna vi inchi vingi, ni kwamba viongozi wetu hawakatai. Wanakubali tu. Lakini sisi ni madodoki? Dodoki ulitumbukize katika maji, hata yenye takataka, linazoa tu!
Kusema kweli, duniani watu wanafikiri kwamba labda sisi ni masikini. Lakini umasikini mbaya kulio wote ni umasikini wa mawazo. Ni mbaya sana. Duniani kuna kujitegemea na kutegemea. Unaweza kutegemea, lakini kutegemea kokote ni kubaya sana. Kwa hali yo yote ile, kutegemea kubaya kupita kote kabisa ni kutegemea mtu mwingine kwa mawazo. Ni kwa ovyo sana kunakunyima utu  wako. 
Watu tunaafikiana na wazo. Lakini mawazo ambayo wazi wazi ni ya kijinga lazima tuyakatae. Kwa sababu mtu mwenye akili akikupa mawazo ya kipumbavu, usipoyakataa, atakudharau. Narudia, mtu ye yote mwenye akili akikupa mawazo ya kipumbavu na wewe una akili na unajua ni ya kipumbavu na ukayakubali, atakudharau. Sasa hatuwezi tukakubali mambo ya kipumbavu Tanzania. 
Shirika la Fedha la Kimataifa sio Wizara va Fedha ya Kimataifa
Ukiuliza kwa nini, wanasema “Mwalimu Benki ya Dunia”. Benki ya Dunia hawa nani?. Mungu gani mpya huyu anaitwa Benki ya Dunia? Vile vile wanasema, “Mwalimu, tumebanwa na Shirika la Fedha la Kimataifa”. Hawa ndio nani? Hawa nimeanza kuwasema mwaka 1980 nikasema “tangu lini Shirika la Fedha la Kimaatifa limegeuzwa kuwa Wizara ya Fedha ya Kimataifa?” Swali hili nililiuliza mwaka themanini wakati nilikuwa nadhani nitaacha uongozi wa nchi yetu. Kwa nini, kama kweli sisi watu wazima na akili zetu, tunakubali mambo ya kipumbavu tunasema, ‘tuuze mashirika yetu’. Tulianza na mashirika ambayo hayana faida tukasema; “uzeni hili halina maana’. 
Lakini, taratibu tukasema, ‘mashirika yenye faida sasa uzeni’ na tunaanza kuyauza. Hata hivyo, tunauliza “haya tunayauza kwa misingi gani maana hata chama chetu kinasema tusiyauze” wanajibu, “ah! Mwalimu, tumebanwa na Shirika Ia Fedha la Kimataifa”. Mungu mpya nani huyu? Hivi ni kweli hatuwezi kukataa sasa? Kwa nini nasema hivi ni kwa sababu tayari tunayo matatizo mengi katika uchumi, afya na huduma za umma zote. Mambo yanakwenda ovyo. Ukiuliza kwa nini, wanajibu “Shirika la Fedha la Kimataifa Mzee”. Ni kitu gani hicho? 
Serikali haihimizi ulipaji kodi
Wamewahi kunijia vijana wetu wamiliki wa viwanda hapa nchini wakati bado ningali Mwenyekiti wa CCM wakaniambia: “Mwalimu, wafanya biashara hawa si wafanya biashara ni walanguzi”. Vile vile, wafanyabiashara wenye viwanda vyao walinifuata pale Msasani, wakati ningali Mwenyekiti wa CCM, wakaniambia: Mwalimu, tunaomba serikali ikusanye kodi, hilo tu. Hatuombi serikali itulinde. Isilinde viwanda vyetu kwa namna nyingine yo yote isipokuwa ikusanye kodi basi. Kama ikikusanya kodi, basi nguo zinazoingia kutoka nchi jirani, zisiingie bila kulipa kodi. Zilipe kodi, hatuombi zaidi ya hapo. Zikilipa kodi, basi tutashindana. Zisipolipa kodi, bidhaa tunazoziona zote hizi hazilipi kodi. Hatuwezi kushindana hata kidogo. Tutakufa. Wakubwa hawa hatuwawezi. Wataleta vitu hapa, kwanza ni rahisi zaidi kuliko vyetu. Pili, visilipe kodi forodhani, viingie nchini hivi hivi! Viwanda vyetu vitakufa! Sasa nasema, angalao serikali ichukue kodi na kodi ipo, na wala sisemi waongeze kodi kwani vipimo vile vya kodi vipo. Tunachoomba serikali itoze tu.
“Serikali”, wananiambia, “ zaidi ya miaka mitatu tokea mwaka 1995 imepoteza shilingi sitini bilioni taslim”. Nimeambiwa hilo zaidi ya mara tatu na wafanyabiashara “Serikali inapoteza shilingi sitini bilioni kwa kutokusaya kodi”. Mara tatu! Kwa hiyo, safari hii niliposikia wakubwa wanasema mmepoteza sabini bilioni miaka mitatu au minne iliyopita, sikushangaa.
Hamkusanyi kodi kwa nini? Kwa kutokusanya kodi, mnaviua viwanda vyetu vya nyumbani hapa. Lakini, mnafanya madhambi mengine makubwa zaidi kuliko kuviua viwanda vyetu. Mnasemaje, maana kisingizio hiki cha kusema ni Shirika la Fedha la Kimataifa na Benki ya Dunia hakipo tena kwani baadhi yao ndio wanaosema “kusanyeni kodi”. Hivi kisingizio hiki cha kwamba kila jambo ni Shirika la. Fedha la Kimataifa na Benki ya Dunia ni cha kweli mpaka leo? Mbona wao tena ndio wanaowambieni “Kusanyeni kodi msipokusanya, tunaweza tukafikiria kuchukua hatua kama mnadhani ni mambo ya utani hivi. Sasa kusanyeni kodi!” 

TUNAKWENDA WAPI? - VIONGOZI TUNAOWATAKA
Naeleza baadhi ya matatizo ambayo viongozi tutakaowachagua tuwe na hakika iwapo wanayaona hivi kama sisi tunavyoyaona. Yanawauma kama sisi yanavyotuuma na kwamba, watakapofika hapo wanapopataka watusaidie kuyatatua. Wanayaona, yanawakera na hata watakapofika hapo, hicho ndicho kitakachowasukuma kutaka kuwa marais wetu na wabunge wetu. Marekani walikuwa na rais wao kijana mmoja mdogo anaitwa John Kennedy. Walimpiga risasi. Marekani nao ni watu wa ajabu sana! Vijana walilaani tukio hilo kwa kuwa walikuwa wanadhani wamemchagua rais wa umri wa kama miaka arobaini na mitatu au minne hivi. Sasa huyo ni kijana, hata kwa hapa Tanzania leo ni kijana. Alipochaguliwa na Marekani akawa Rais wao. Katika hotuba yake ya kwanza kabisa aliwambia wananchi wenzake, hasa vijana “Usiulize Marekani itakufanyia nini, jiulize wewe utaifanyia nini Marekani?”. 

Kila anayetaka kuwa mgombea wa urais/ubunge ajiulize ataifanyia nini nchi yake
Tunataka mtu anayetaka kuwa rais wetu ajiulize anataka kuifanyia nini nchi yetu na sio nchi yetu itamfanyia nini. Na tunataka swali hilo ajiulize kila mtu anayetaka kuwa mgombea wa chama cho chote kuwa mbunge/rais: “Kwa nini, kwa dhati kabisa, anaumwa na umasikini wetu na umasikini huo ndio unaomsukuma ashughulike na mambo haya ya siasa katika ngazi hiyo ama ya ubunge ama ya urais”. Kama sivyo, hatufai! 
Mtu hapakimbilii Ikulu: Hakuna Biashara Ikulu
Mtu anayetaka kwenda Ikulu kutaka faida ye yote Ikulu pale hatufai hata kidogo. Wananchi, mimi nimekaa pale Ikulu kwa muda mrefu zaidi kuliko mwingine ye yote, wala sidhani kuna mtu mwingine anaweza kuzidi muda huo. Tayari hapa tumeweka sheria. Kwa mujibu wa sheria, mtu hawezi tena kukaa Ikulu zaidi ya miaka kumi, kipindi ambacho hata hakijafikia nusu ya kipindi nilichokaa. Mimi nimekaa miaka ishirini na tatu!
Najua, kwa mtu halisi kabisa, Ikulu ni mzigo! Hupakimbilii! Si mahali pa kupakimbilia hata kidogo; huwezi kupakimbilia Ikulu. Unapakimbilia kwenda kutafuta nini? Ni mgogoro; ni mzigo mkubwa kabisa! Ukipita barabarani, unakuta watu wana njaa, unaona ni mzigo wako huo. Pazito pale! Huwezi kupakimbilia na watu safi hawapakimbilii. Ukiona mtu anapakimbilia, na hasa anapotumia tumia vipesa kwenda Ikulu, huyo ni mtu wa kuogopa kama ukoma!
Mtu ye yote anayeonekana anapenda sana kwenda Ikulu na hata yupo tayari kununua kura ili kumwezesha kufika Ikulu ni wa kumkwepa kama ukoma. Kwanza, hizo fedha kapata wapi. Mtanzania wa leo hawezi kununua watu bila kwanza yeye kununuliwa. Na kama kanunuliwa, atataka kuzilipaje? Kazipata wapi? Watanzania wote ni masikini tu. Mtanzania anaomba urais wetu kwa hela! Amezipata wapi? 
Pili, kama hajanunuliwa, kazipata wapi? Kama kakopa, atarudishaje? Ikulu pana biashara gani mtu akope mamilioni halafu aende ayalipe kwa biashara ya Ikulu? Ikulu mimi nimekaa kwa muda wa miaka ishrini na mitatu. Ikulu ni mahali pazito. Kuna biashara gani Ikulu? 
Rushwa na Matumizi ya Fedha Bila Utaratiba Wakati wa Chaguzi
Sisi Waafrika ni watu wa ajabu sana. Unajua ni wadogo, lakini nasema, ni udogo wa mawazo. Umaskini wa mawazo ni umasikini mbaya kupita wote. Unaweza ukawa na almasi mfukoni, akaja tapeli na kijiwe kimetengenezwa kama almasi akakuambia “ebu tuone almasi yako. Bwana aa! Hii ya kwako sio almasi ni chupa tu, almasi ni hii. Kwanza nipe bwana.” Mkabadilishana. Yeye akachukua almasi yako na akakuachia kichupa na ukatoka hapo unashangilia kama zuzu!
Sisi hapa Tanzania tulikuwa tumeanza utaratibu ambao ukitumia fedha nje ya fedha za chama na serikali na ukatumia fedha zako mwenywe katika uchaguzi, tunakutoa. Hufai! Huo ndio ulikuwa utaratibu wetu. Tulikuwa tunakuuliza: “hii nchi ya masikini, wewe mwenzetu una mali umeipata wapi?”
Mali, kwa wakati huo, kwetu sisi ilikuwa ni sifa ya kukunyang’anya uwezo wa kugombea uongozi Tanzania. Tulijua kwamba, kama una mali, utaficha. Leo watu wanasema waziwazi: “Mwalimu uchaguzi wa mwaka huu utapitishwaje?”
Marekani wanatumia fedha nyingi sana katika uchaguzi. Nyingi sana! Kama Marekani sasa hivi wanazungumza watunge sheria inayofanana na ile mliyoitupa ninyi mnadhani kwa sababu ni mawazo ya masikini, haina maana. Wakubwa wanayafikiria mawazo hayo sasa hivi. Marekani wanafikiria uwezekano sasa wa kutunga sheria itakayoweka utaratibu wa fedha za ugombeaji kutokana na mfuko mmoja baada ya kugundua kwamba inapokuwa holela na kila mtu akiachiwa lwake, inavuruga. Inaleta rushwa kubwa kabisa. Unanunuliwa urais na unaweza kununuliwa na fedha za wauza bangi na wauza baa. Wauza bangi wanaiona hatari hiyo, ninyi haa!
Hapa tulikuwa na utaratibu mzuri kabisa tuliouanzisha mlioutupa, mnafikiri, sisi mwaka huu fedha tu! Uchaguzi wa fedha, mtazipata wapi? Mimi nimetoka juzi tu, mara mmetajirika kiasi hiki! Waswahili hee! Kumbe mnaweza kutajirika zaidi kwa haraka hivyo? Sasa kama mnao uwezo wa kutajirika, nawambieni ‘Fanya wote tutajirike. Hivi mtajirike peke yenu, tutajirike wote”. Wapi! Ni rahisi sana watu wachache kutajirika.
Tunataka Serikali inayotoza kodi
Kwa hiyo, naserna sasa hivi mimi sijali kabisa na wala msifikiri tena napinga watu wanaotaka uhuru wa kujipatia mali. Tunataka serikali itakayotoza kodi. Tulikuwa na viserikali vya rafiki zetu za Skandinavia vinavyoongozwa na watu wanaojali maslahi ya umma. Vinatoza kodi matajiri, halafu mapato hayo yanasambazwa kwa faida ya wote. Hata hapa fanyeni hivyo. Lakini isiwe ni kukusanya kodi na halafu, kilicho chetu mnataka kukiuza. Hata hicho muuziane, halafu mpate pesa na hizo pesa zenu wala msilipe kodi! Hii ndio kazi tuliyowapeleka Ikulu?
Sifa za ziada za viongozi
Nilipokuwa Dar es Salaam, nilieleza mahala fulani kwamba watu wanaotaka kutuongoza wawe angalau na sifa hizi na hizi. Sasa nasema hata wakiwa nazo bado tutawauliza: “sifa mnazo, lakini mnakwenda kufanya nini?”  Hata nikiwa na watano wenye sifa nzuri bado nitasema: “Ninyi watano mna sifa nzuri kabisa, mimi sioni kama mna kasoro lakini bado nitawauliza hasa mnakwenda kutafuta nini Ikulu. Uniambie kwa dhati ya moyo wako kinakuuma nini kwamba unaweza kweli ukaumwa kabisa”. Halafu ukasema: “Mwalimu, Ikulu sipapendi. Ikulu siyo tatizo. Kama mambo yanakwenda ovyo ovyo utaacha tu?
Zile sifa nilizozitamka hazitoshi: kwamba lazima uwe Mtanzania na unaheshimu Tanzania. Maana tunatafuta rais wa Tanzania na wala hatutafuti wasifu wa Rais wa Tanzania. Tuna miezi saba uwe umezipata zile tano na kuendelea. Hata hivyo, bado tutawauliza mambo ya uchumi, viwanda na shule unavyoyaelewa. Mambo ya afya, ninyi mnayajua yote. Hospitali zetu, hali yake ya sasa hivi mnaielewa inaendaje endaje na kama mnaelewa ninyi unaionaje? Unaona raha tu? Maana sisi ni watu wa sera ya kuchangia. Sawa. Lakini wewe umechangia mara ngapi? Hebu nenda katika hospitali moja uone watu wanavyochangia.
 Tunataka kufikiria kwa msingi kwamba kitu kimoja tunachotaka kuelewa ni hali ya matatizo yetu yalivyo sasa. Hii ni kwa sababu awamu ya kwanza, awamu yangu mimi, imefanya mema na imefanya ya kijinga. Yale ya kijinga, mnayaacha. Lazima yanaachwa. Ubaya wenu ni kwamba mnayaacha mema na mnachukua ya kijinga. 
Miaka ishirini na tatu, bwana, lazima tumefanya makosa. Pale, bwana, hatukuwa na wasomi wengi, ujuzi wala cho chote. Tulikuwa tunahangaika tu. Kama watu hamjui kuogelea, mnatupwa kwenye maji, mnahangaika kuogelea, lazima mtafanya makosa. Tusifanye makosa kwani sisi ni malaika? Awamu ya kwanza ina mambo fulani fulani na hasa ya msingi na mengine ya utekelezaji mazuri, mnaendelea nayo. Mengine ya utekelezaji ya ovyo ovyo, mnayachilia mbali mnaanzia hapo tena.
 Ila la ajabu ni kwamba hata ya msingi mnayawekea alama ya kuuliza. Mimi sikudhani kama ya msingi yalikuwa na matatizo, Nilidhani mambo yetu ya utekelezaji yana matatizo mengi hivi ya kusikilizana, hata ya msingi. Sasa watu wataanza kugombana katika misingi ya ukabila, udini na mambo mengine ya kijinga kabisa.
Kwa hiyo, nasema, awamu ya pili mnaanza na mengine mnaongeza hapo. Awamu ya pili nayo inafanya makosa yake, itafanya mema yake. Yale mema, ndiyo mnayoendelea nayo; mnaendelea na yale mema yake. Yale mabaya mnayaacha kama yalikuwapo ya msingi yamesahauliwa mnayarudia. Kutoyarudia yale ya msingi, mtapotea tu. Mnafanya hivyo halafu mnaendelea. 
Mimi nataka kujua kama viongozi wetu wa sasa hivi wanaotaka kuingia katika awamu ya tatu ya uongozi wanayaelewa hivyo na tutaelewana hivyo au wanafikiri uongozi ni biashara tu! Je wanaotaka kutuongoza wanaweza, kwanza, kuelezea tulikuwa wapi, tuko wapi, tunataka kwenda wapi? Pili, je wanao uwezo wa kutupeleka kule tunakotaka kwenda? Tatu, watatushirikishaje kule ili na sisi tusaidiane kwenda huko? Hiyo ndiyo kazi iliyobaki. Pimeni Sana!

HOJA YA WAGOMBEA BINAFSI
Nataka kusema kauli ya mwisho kuhusu sheria ya uchaguzi ilivyo sasa hivi. Ninalo tatizo moja. Hili nataka kulisema kwa sababu nadhani ni la msingi kidogo. Tulipokubali tuwe na vyama vingi vya siasa tulisema kwamba hivi vyama vingi vina migogoro. Mnaweza mkawa na chama cha dini, kabila, mkoa kinaitwa chama cha Mbeya ama katika nchi kikaitwa Zanzibar au Tanganyika tu. Tulisema sisi hapana ni taifa changa. Lazima tujihadhari na chama kinachoweza kutugawa. Tunataka chama kinachokubali umoja. Kwa hiyo, tukakataa vyama vya udini, ukabila na vya kutenganisha Tanzania. Tanzania tukaigawa, sijui inaitwa Tanganyika na Zanzibar, sijui inaitwa Tanganyika na Tanzania Zanzibar. Hapana tukatae vyama vya namna hiyo.
Kwa hiyo, tuliamua kwamba yawepo masharti ya kisheria yanayozuia vyama kuwa vya namna hiyo. Hii ni kulinda umoja ili tujenge upya kwa kuwa bado tu wachanga mno. Basi, sheria hiyo ndivyo ilivyotungwa na ndivyo ilivyo. Huwezi kuanzisha chama ambacho kinakiuka upande huo wa sheria. Hata hivyo, mimi nadhani sheria imekosea kuzuia wagombea binafsi. 
Nataka nieleze sababu kwa nini nadhani kukosea huku ni kwa msingi na si kwa juu juu. Hili jambo limekosewa ni la msingi. Ndiyo maana napenda kulisema kwa nini ni la msingi. Linahusu haki yangu na yako ya kupiga kura. Hii ni haki ya uraia. Madhali wewe ni raia wa Tanzania [huna kichaa, huko gerezani, umetimiza umri unaotakiwa wa miaka kumi na minane] una haki ya kupiga kura. Ni haki yako ya uraia. Iko mfukoni mwako! Hii haki ya kuomba upigiwe kura pia ni haki ya uraia; ni haki yako. Unaomba ubunge au cho chote kile upigiwe kura na hata unaomba urais, ni haki yako ya uraia; huwezi kunyimwa maadam wewe ni raia wa Tanzania kisisasa una haki ya kuomba uwe rais.
 Ukiwa katika chama ama hupo katika chama. Unayo haki inayotokana na uraia wako ya kupiga kura na ya kupigiwa kura ambayo haiwezi kudaiwa na mtu ambaye si raia wa Tanzania. 
Aidha, raia wa Tanzania hawezi akanyang’anywa haki hii ya kuomba uongozi wa nchi yake tangu ngazi ya kijiji mpaka ngazi ya taifa. Iwapo wapo wasio na uwezo huo wa kutaka kuwa rais, hiyo ni shauri nyingine. Lakini haki ninayo wakataohukumu kama nina uwezo au sina uwezo ni wananchi. Mimi sasa hivi niko hapa nawaelezeni jinsi ya kuwahukumu wenye uwezo na wasio na uwezo. Lakini sisemi hawana haki. Haki hiyo ndiyo inayowafanya ninyi wafanyakazi, ninyi wafanyakazi mnazo haki za wafanyakazi, nikasema “lakini mmoja mmoja hatuwezi, lazima tushirikiane”. Kwa hiyo, mnashirikiana wote kwa pamoja. Hivyo ni vizuri zaidi.
Tunasema ni vizuri tuiombe na tujaribu kuitumia haki ile ya kuunda vyama. Mnaweza mkaunda vyama. Sijui wangapi wameweza kuingia katika vyama maana tunayo haki hiyo. Sasa hivi mnasema viko kumi na vitatu. Sina hakika kama vimechukua Watanzania wote. Watanzania wengine hawamo CCM, hawapo wapi na hawana chama chochote. Hata hivyo, nikikataa kuingia katika chama isiwe sababu ya kuninyang’anya haki yangu ya kupiga an kupigiwa kura. Ninayo tu na naweza nikaamua kuitumia mwenyewe tu! 
Lakini, msije mkanielewa vibaya kuhusu kile ninachotaka kusema kwamba raia ye yote wa Tanzania anaweza kusema “mimi mgombea urais”. Tutamwambia: “Ah! Unaweza bwana peke yako kweli utasimama hivi kwa Tanzania peke yako utapitapita huku na kule watakupigia kura?” 
Unaweza kumlaumu na kumhukumu useme: “Wewe ni mjinga”. Lakini huwezi kusema huna haki hiyo. Ni haki yake. Anaweza kuwa mjinga. Labda kuwa ni mtu anayedhani kwamba “Watanzania wakishaona uso wangu, hata kama sina kitu, watanichagua”. Anaweza kuwa si mgombea makini, lakini ni haki yake.
Sasa sheria inawanyima raia wa Tanzania haki hiyo. Mtu mmoja akaenda mahakamani kudai haki hiyo akasema “sheria hii si haki”. Jaji mmoja akahukumu akasema “naam, si haki”. Mimi nakubaliana na maamuzi yale ya Jaji kabisa. Jaji alikuwa sahihi, hata kama alihukumu vile kwa bahati, kwa sababu haki hii iko katika Katiba. Ingekuwa haiko katika Katiba, ungekuwapo ubishi, lakini imo ndani ya Katiba. Kwa hiyo, Jaji akasema: “Naam, hawawezi kumnyima haki”. 
Sasa serikali watafanyaje? Badala ya kukubali uamuzi wa Jaji, kwa kweli walichokifanya kwa kweli ni kuifuta. Ndiyo, hamwezi kufuta haki za raia. Hamna uwezo wa kufuta haki za raia. Ndugu Waziri, hamna uwezo wa kufuta haki za raia. Hamuwezi kweli kabisa kabisa. Serikali haiwezi ikasema haki hii inakera kidogo. Inakera kisiasa tu lakini na sio kimaadili. Sheria hii inawakera kisiasa halafu mnaifuta, mtatunga kesho sheria nyingine itawakera, mtaifuta. MTAFUTA NGAPI?
Sasa mimi nina ugomvi huo. Na ni ugomvi wa kasoro kubwa, si kasoro ndogo. Ingekuwa kasoro ndogo, nisingejua. Hatuwezi kumnyima raia haki yake. Mimi napenda watu watumie hii haki yao ndani ya vyama. Kama vile nilivyosema, mfanyakazi unayo haki ya mshahara na kudai mshahara mzuri. Unaweza kudai peke yako tu hivyo hivyo. Unayo haki, ijapokuwa haiwezi kukupa nguvu. Mfanyakazi kutoingia kwenye chama hakumpotezei haki yake ya kudai mshahara mzuri hata kidogo. Kunampunguzia ile nguvu ya kufanikiwa peke yake; Lakini, anayo haki bado, inabaki ni haki yake. Huyu raia wa Tanzania akisimama peke yake tu, hana uwezo ule ule kama angekuwa ana simama na wengine.
Tujifunze kutoka historia ya uchaguzi wa 1961
Sasa mfano mmoja nautumia mwisho kabisa. Mwaka wa elfu moja tisa mia na siti na moja tulikuwa na uchaguzi mkuu. Akatupinga kijana wetu mmoja anaitwa Herman Sarwatt. Ndiyo, si ulikuwa uchaguzi wa vyama vingi? TANU ilikuwa imechukua viti vingi bila kupingwa. Kiti cha Mbulu tulikuwa tumemweka Chief mmoja anaitwa Chief Amri Dodo. Mwanàchama wetu mmoja alikuwa anaitwa Herman Sarwatt akasema. Alaa! Hiki chama changu hakina akili hata kidogo. Hawa viongozi wangu hawana, akili! Hawa machifu ndio zamani wakitaka kutufunga wakati tukigombana na mkoloni. Leo wanamchukua Chief Dodo aliyetaka kutufunga sisi ndiye awe mbunge wetu katika jimbo la Mbulu?
Sasa sisi tulikuwa tumekwisha kumchukua huyu kuwa ndiye mgombea rasmi wa TANU. Kijana yule akatupinga.  Mimi nilitokea hapa Mbeya na nikasafiri kutoka Mbeya kwenda Mbulu kumteiti yule mgombea wa TANU. Nikashindwa. 
Wananchi wa Mbulu hawana uanachama tena, wengi tu wakasema “TANU wamekosea”. Wakampa kura Sarwatt. Wakafanya hivyo, Mwanachama wa TANU akasimama mwenyewe akatushinda! Ilikuwa haki yake. Hatukuiondoa. 
Mimi nadhani kwamba kwa kuwa sasa tunarudisha vyama vingi, vile vile tunarudisha haki zote zile zilizokuwapo za raia pamoja na haki; siyo haki ya kuunda vyama bali pia wagombea binafsi kusimama kama Sarwatt alivyofanya. 
Mwisho 
SasaNdugu Waheshimiwa, nawashukuru sana, tena sana, kwa kunipa nafasi na kwa kunipokea mlivyonipokea. Mwaka huu ni mwaka ambao una umuhimu huo. Basi tuendelee kusaidiana jinsi ya kuweza kupata matokeo ya uchaguzi wa wabunge na rais ambao utatufikisha huko tunakotaka kwenda.
Ahsanteni Sana.